LHRC Wampinga Waziri Nchemba Matumizi ya Viboko Shuleni

Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), kimetofautiana na kauli ya Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk. Mwigulu Nchemba ya kutaka walimu kutumia adhabu ya fimbo kuweka nidhamu kwa wanafunzi shuleni

Akizungumza katika harambee ya ujenzi wa mabweni ya Shule ya Sekondari Lulumba Wilaya ya Iramba mkoani Singida, Dk. Nchemba alisema walimu wanatumia fimbo kunyoosha nidhamu za wanafunzi, ili kutengeneza hatima ya nchi.

Alisema wakati walimu wakitekeleza majukumu yao ikiwamo kunyoosha nidhamu kwa wanafunzi kwa kutumia fimbo, wapo baadhi ya watu wamekuwa wakiwalalamikia na kuwataka wawaache watekeleze majukumu yao.

“Wakati walimu wananyoosha nidhamu za wanafunzi, wapo watu wengine huwalalamikia tu, na hawajui kwamba kinachofanyika ni kwa manufaa yetu. 

"Niwaombe kwenye kutumia mifano tumieni mifano na kwenye kutumia fimbo fanyeni hivyo, ili kutengeneza taswira ya nchi yetu,” alisema Dk. Mwigulu.

Akizungumzia kauli hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Dk. Hellen Kijo Bisimba, amesema kutumia fimbo kwa mwanafunzi hakuwezi kusaidia kumjengea nidhamu.

Pia, amesema kutumia adhabu hiyo kunaweza kuwa chanzo cha kurudisha nyuma maendeleo yao kielimu.

“Ni kweli kwamba walimu wanapaswa kuachwa watekeleze majukumu yao bila kuingiliwa, lakini linapokuja jambo la adhabu au kujenga nidhamu kwa wanafunzi lazima uangaliwe mfumo unaotumika,” alisema Dk. Kijo Bisimba na kuongeza:

“Zipo adhabu ambazo mwanafunzi anaweza kupewa akikosa, lakini si kwa kuchapwa fimbo. Unaweza ukafikiri ukimchapa ndio unamjenga, lakini kumbe ndio unambomoa zaidi. 

"Nasema hivyo kwa sababu unapoanza kumchapa mwanafunzi hawezi kufanya vizuri tena darasani. Mimi namuomba waziri a-deal (ashughulike) na mambo ya wizara yake, ya elimu ayaache.”

Post a Comment

Kwa maoni na ushauri weka comment yako hapo chini:

Previous Post Next Post