Kombe la Dunia 2018 Urusi: Ubelgiji na Senegal washinda mechi za maandalizi


Romelu Lukaku alifunga mabao mawili na kuwawezesha Ubelgiji kupata ushindi mkubwa wa 4-1 dhidi ya Costa Rica, nao Senegal wakashinda 2-0 dhidi ya Korea Kusini mechi zao za mwisho ya kujiandaa kwa Kombe la Dunia.
Ubelgiji, ambao wamo Kundi G pamoja na England walikuwa bila beki wao aliyeumia Vincent Kompany.
Kiungo wao Eden Hazard pia alionekana kuchechemea na kuondoka uwanjani dakika ya 70.
Bryan Luiz alikuwa amewaweka mbele Costa Rica dakika ya 24 kabla ya mshambuliaji wa Napoli Dries Mertens kusawazisha.
Romelu Lukaku sasa amefunga mabao 36 akichezea timu ya taifa ya Ubelgiji
Lukaku kisha alifunga kabla ya mapumziko na kipindi cha pili.
Baadaye alichangia bao la Michy Batshuayi la nne kwa Ubelgiji mechi hiyo iliyochezewa Brussels.
Ubelgiji wataanza kampeni yao Kombe la Dunia dhidi ya Panama Jumatatu nao Costa Rica waanze kwa kukutana na Serbia mechi yao ya kwanza Kundi E Jumapili.
Mkufunzi mkuu wa Ubelgiji Roberto Martinez amesema Hazard aliondoka uwanjani kutokana na kutatizwa na mguu lakini akaongeza kwamb: "Hakuna sababu ya kuwa na wasiwasi.
"Nilifurahia sana uchezaji wake. Alikuwa makini na mwenye nguvu, alicheza vyema sana."
Bao la Luiz lilitokana na kutomakinika kwa beki wa kati wa Tottenham Jan Vertonghen.
Ubelgiji kisha walidhibiti mechi hiyo, ambapo Hazard, Kevin de Bruyne na Mertens waliwatatiza sana mabeki wa Costa Rica.
Moussa Konate alifunga mabao 13 katika Ligue 1
Senegal nao walikamilisha maandalizi yao kwa ushindi wa 2-0 dhidi ya Korea Kusini mechi iliyochezewa uwanja usio na mashabiki Austria.
Moussa Konate alifungia Senegal bao la pili baada ya wapinzani wao kujifunga kupitia Kim Young-Gwon dakika ya 67.
Mshambuliaji huyo wa Amiens alifunga kupitia mkwaju wa penalti na kuwahakikisha vijana hao walio chini ya f Aliou Cisse ushindi.
Korea Kusini wataanza kampeni yao Kombe la Dunia kwa mechi dhidi ya Sweden Kundi F 18 Juni nao Senegal wakutane na Poland Kundi H Jumanne.

Post a Comment

Kwa maoni na ushauri weka comment yako hapo chini:

Previous Post Next Post