Chanzo, kifo cha Isack Gamba baada ya uchunguzi

Aliyekuwa mtangazaji wa zamani wa ITV, Radio One na baadaye Idhaa ya Kiswahili ya  DW, Isack Muyenjwa Gamba ameagwa leo katika viwanja vya Hospitali ya Jeshi Lugola jijini Dar es salaam, tayari mwili wake umesafirishwa kuelekea jijini Mwanza na baadaye Bunda kwaajili ya maziko.


Isack Gamba enzi za uhai wake.
Akisoma taarifa fupi ya marehemu, mtangazaji nguli nchini ambaye amewahi pia kufanya kazi na Gamba, Regina Mziwanda amesema kuwa kuwa chanzo cha kifo chake kilichogundulika kwenye uchunguzi wa madaktari nchini Ujerumani kimetajwa kuwa ni kuvuja kwa damu kwenye ubongo kutokana na shinikizo la damu.
"Baada ya uchunguzi wa hospitali nchini Ujerumani, iligundulika kuwa kifo chake kimesababisahwa na kuvuja kwa damu kwenye ubongo kulikosababishwa na shinikizo la damu", amesema Regina.
Awali akitoa salamu za mkoa, Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, Paul Makonda amewataka wanahabari kuendeleza umoja na mshikamano katika nyakati zote na kusema kuwa marehemu Gamba amempa umaarufu nchini Ujerumani, kwani alikuwa akihabarisha kila tukio lilikokuwa likitokea Dar es salaam nchini humo.
"Majira na nyakati anazijua Mungu, lakini sisi tunapaswa kujiandaa wakati wowote ule kwa maana hatujui siku wala saa ya kuitwa kwetu, niwape pole waandishi wote wa habari na niwashukuru kwa heshima mliompa Isack", amesema Makonda.
Mwili wa Gamba utaagwa na wanahabari na wadau wa tasnia ya habari jijini Mwanza kesho saa tano asubuhi, na baadaye kuelekea wilayani Bunda mkoani Mara ambako ndiko alikozaliwa kwaajili ya maziko.
Taarifa juu ya kifo cha mtangazaji huyo nguli wa zamani zilisambaa usiku wa Oktoba 18, zikieleza kuwa alikutwa akiwa amefariki nyumbani kwake mjini Bonn Ujerumani ambapo kabla ya kubainika kwa kifo chake mtangazaji huyo hakuonekana ofisini kwa takribani siku tatu.

Post a Comment

Kwa maoni na ushauri weka comment yako hapo chini:

Previous Post Next Post