Simulizi kwa ufupi kuhusu historia ya Messi


Messi aliishi kwenye nyumba iliyojengwa na Baba kwa kushirikiana na Babu yao. Nyumba hii ilijengwa kwa mikono ya Wazazi wao wenyewe. Nimezikumbuka zile nyumba za Msonge Rombo ambazo mnajenga kwa siku moja tena kwa jitihada zenu wenyewe.

Dada yake Messi pamoja na Mama yao waliishi kwenye nyumba hiyo mpaka mwaka 2010, kwa maelezo ya Sebastian Fest na Alexandre Julliard katika kitabu chao cha Misterio Messi: Los Secretos del Mejor Jugador del Mundo.

Nukuu
“Mwanamke mwenye miaka 30 na zaidi anatoka nje ninapogonga mlango. Cha ajabu haongei chochote. Anatokea mwanamke mwingine nyumba ya pili aliyejitambulisha kwa jina la Lucia. Nikamuuliza unamjua vipi bwana mdogo Messi akanijubu ” Muy tranquilo,” Maana yake namjua alikuwa MDOGO SANA.

Tatizo yule mtoto alikuwa MSUMBUFU MNO. Yaani dada yangu alikuwa halali. Alituharibia ukuta wetu kwa sababu ya mipira yake. Kila saa alipiga mpira ukutani. Dada yangu alikuwa anakimbizana nae. Kumpiga tulishindwa maana kalikuwa kadogo inafika mahali unakaonea hata huruma.

Ndugu yangu uliyepo Kasulu, Kibondo, Ifunda, Ikwiriri umeacha historia gani mtaani kwenu? Sasa hivi tukirudi mtaani kwenu tukikuulizia watatuambia ulikuwa nani? Hujabadilika? Bado upo vile vile? Kwanini? Huna historia? Amini tu kwamba Historia yako ipo. Jenga mafanikio kwanza kila mtu atakuongelea kwa lugha tofauti. Kwasasa kwa kuwa huna jipya kila mtu atakupouzia. Tena wataongelea mabaya yako tu.

Chipukizi Leo Messi alijiunga na klabu ya mtaani kwao ijulikanayo Newell’s Old Boys ilijukana kwa utani kama “Nuls,”. Wakati huo alikuwa na miaka 6 tu. Siku kama ya leo Messi anatimiza siku yake ya kuzaliwa. Leo Messi huenda siku yake ya kuzaliwa akaikumbuka siku alipotimiza miaka 6 wakati wa sherehe yake ya Kuzaliwa Shangazi na mjomba wake walimpelekea jezi ya rangi nyekundu na nyeusi ambayo ilikuwa ikitumia klabu ya Newells.

Wakati ule alikuwa akimlilia kaka yake mkubwa aliyekuwa akiichezea klabu hiyo amepeleke uwanjani nae akacheze nao. Changamoto kubwa ilikuwa hali yake ya afya.

Mwaka 1993 alibahatika kwenda uwanjani kuitazama klabu yake hiyo aliyokuwa anaipenda. Wakati huo Newells ilikuwa inacheza uwanja wa Rosario. Nguli wa soka duniani Diego Maradona wakati huo alikuwa akiichezea klabu hiyo. Messi alifurahia sana kumuona Maradona akisakata kabumbu. Hivi Majuzi tuliona Maradona akiwa uwanjani akijaribu kumtia Messi moyo alipokuwa na timu yake ya taifa kule Urusi dhidi ya Croatia.

Maisha ni kujituma na kupambana na kila changamoto unayokumbana nayo katika maisha. Mchezo wake wa kwanza kabisa na klabu ya watoto ya Newell ilishinda mabao 6-0 huku Leo Messi akifunga mabao manne licha ya kwamba alikuwa na umbo dogo na alidhohofu sana mwili.

Wadau wengi wa soka walishangazwa sana na kipaji cha bwana mdogo yule. Mtaani alianza kutajwa tajwa kutokana na muonekanao wake na yale aliyokuwa akiyafanya uwanjani. Waliamua kumpachika jina la “La Maquina del ’87,” au “The Machine of ’87,” Maanake Mashine ya 1987 ikiwa ndio mwaka aliozaliwa.

Huenda katika maisha kuna udhaifu ulio nao. Huenda jamii inakuchukulia tofauti. Huenda wewe ni Albino, huenda una ulemavu, usikimbilie kuwa omba omba, usilalalamike wala kulialia, Mweke Mungu mbele mwambie naomba mwaka kesho niwe sehemu fulani. Inuka, Nenda, kafanye, jitetee, pambana na hakikisha unakuwa na nidhamu na uchu wa kutaka kufanikiwa. Haijalishi unawakera watu vipi lakini hakikisha unatimiza lengo

Messi alikuwa ukimnyima mpira atalia siku nzima. Shuleni alikuwa anasubiri ule wasaa wa kwenda kucheza mpira tu. Aliwekeza imani yake yote katika soka kwani aliamini kuwa ndio utakaookoa maisha yake. Tunajifunza kitu hapa. Huenda unachokifanya kina dharaulika naa watu. Huenda wazazi au ndugu au majirani au marfiki hata jamaa wanadharau na kupinga harakati zako. Kijana Sauti inayotoka ndani yako ni sauti ya Mungu. Makelele ya chura hayakaushi maji we nenda kachote.

Akiwa na klabu yake, timu yao ilicheza miaka mitatu mfululizo bila kufungwa mchezo wowote katika ligi ya watoto.
Akiwa na umri wa miaka 11 licha ya changamoto ya afya alikuwa na uwezo wa kucheza viwanja vikubwa tena mchana kweupe na jua kali. Wakati fulani waalimu wake waliogopa sana. Tokea alipojiunga na klabu hiyo klabu hiyo ilishinda kila aina ya kombe. Hakuna kombe waliloliacha. Kiujumla Wapinzani walipata tabu sana.

Walipata bahati ya kwenda kucheza hata nje ya nchi kule Peru. Jiulize mtoto wa miaka 11 anakwenda kucheza soka nje ya nchi yao wewe kwanini ukate tamaa na hicho unachokifanya? Mafanikio hayaji kama upepo huandaliwa. Mwaka 2000, Mchezaji mwenzake na Messi ajukikanae kama Franco Falleroni alisema kwa miaka yote 6 klabu yao imefungwa kama mara tatu tu. Gonzalo Mazzia anasema Messi alikuwa hazuiliki. Alikuwa mdogo sana lakini wapinzani walipata tabu. Akipata mpira hatoi pasi lakini uzuri ni kwamba alikuwa hakosei au hapotezi.

“Wakati fulani kipa wetu alikuwa anaweza akakaa hata nje ya goli. Tuliwafunga wapinzani wetu kiasi kwamba mabao yalikuwa yaanzia 10, 15 wakati fulani hata 30. Mpira ulipokuwa hauna ushindani sana Messi aligoma. Alipona wapinzani hawampi changamoto ilikuwa kila akifunga zaidi ya mabao 6 anatushauri wengine tuachane na wapinzani wetu. Mwalimu wetu akaweka utaratibu kwamba timu tukishaifunga mabao 6 mpira unaishia hapo hapo. Shida tuliyokumbana nayo Messi hakupenda kabisa kucheza na wapinzani wazembe wazembe.

Kocha wake wa zamani Adrian Coria anasema kwamna Messi akiwa na miaka 10 alikuwa tayari ameshavuka hata idadi ya mabao 500. Akiwa na miaka 13 alifuatilia na maskauti wa Barcelona. Wakati huo huo River Plate ya huko Argentine ilimfukuzia ikihitaji huduma zake.

Vipi Bro! Kuna wadau wanakudharau unachofanya! Machalii wangu chuga na ndugu zangu wa Dar, wale wa mbeya na popote ulipo Tanzania, wala usiwaze kama unadharaulika. Kule Barcelona wenyewe walimdharau dharau hivi. Hata mkataba wake wa kwanza ulisainiwa kwenye karatasi ya kufutia mikono (Tishu). Sasa hivi ni Mchezaji bora duniani.

Akiwa mdogo alikuwa na uchu wa kufunga sana. Hata kama timu yake ilishinda mabao 10 na yeye hajafunga alikuwa ana hasira sana. Hata nyumbani kwao akirudi alikuwa hawezi kula. Kuna siku aligoma kutoka uwanjani baada ya wenzake kukataa kumpa pasi. Kila mara alitaka mpira upigwe kwake tu. Alikuwa anaweza hata kususa asipopewa mpira. Cha ajabu akipewa huo mpira yeye hatoi pasi kwa wenzake. Alikuwa na uchu wa kushindana. Hayupo tayari kufeli. Hajui neno kushindwa. Ndio maana hata timu yake ya taifa iliposhindwa kufanya vyema aliamua kustaafu.

Falleroni alikuwa rafiki mkubwa sana wa Messi. Messi alihamia kwa Falleron. Muda wote walikuwa wanacheza magemu ya pleisteshen. Falleroni yeye alizaliwa Chabas umbali wa masaa mawili na kiwanja chao cha mazoezi. Baba yake Falleroni alimpenda sana Messi.

Falleron anasema
“Baba yangu alikuwa na gari ya Peugeot 306, Baba almpenda sana Leo. Alikuwa anamfundisha namna ya kuendesha gari. Tulikuwa tunamwekea mito miwili mikubwa kwenye siti ya gari ili aweze kufikia usukani kwani alikuwa mfupi mno”

Messi alizaliwa barrio ukanda wa kusini mwa mji wa Rosario. Ulikuwa mji wa watu hohehahe. Watoto walikuwa wakiona magari wanayakimbilia. Mji huo haukuwa tofauti na mji wa Villa Fiorito, ambao ni mji Nguli Maradona alizaliwa nje ya mji wa Buenos Aires. Maradona alizaliwa mji ambao haukuwa na umeme wala maji. Walikuwa wanauza makopo na maganda ya sigara. Alizaliwa mji ambao ilibidi waokote nguo kwenye magari ya taka ya jiji ili waweze kujisitiri.

Bro ! Umeona Maisha ya Messi na Maradona? Wewe unalalamika huna hela ya bando!

Kwa leo Tuishie Hapa. Naitwa Privaldinho unaweza kunifollow pia Instagram kwa jina hilo hilo. HERI YA KUZALIWA KWA LIONEL MESSI

Post a Comment

Kwa maoni na ushauri weka comment yako hapo chini:

Previous Post Next Post