BOLT AJIANDAA KUIKABILI MO FARAH YA MISR


Bolt ajiandaa kukabili Mo Farah Old Trafford kwa mazoezi na klabu ya Norway

Bingwa wa Olimpiki mara nane Usain Bolt anafanya mazoezi na soka na klabu inayocheza ligi kuu ya Norway, Stromsgodset.

Raia huyo wa Jamaica mwenye umri wa miaka 31 anatarajiwa kucheza mechi ya mazoezi katika ya klabu hiyo na timu ya taifa ya Norway ya wachezaji wa chini ya miaka 19 baadaye wiki hii katika klabu hiyo.

Bolt, anayeshikilia rekodi ya dunia katika mbio za 100m na 200m, tayari amefanya mazoezi na Borussia Dortmund ya Ujerumani na Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini.

"Pengine kuna klabu itaona jambo zuri kwangu na kunipa nafasi," alisema Bolt ambaye anajiandaa kwa mechi ya hisani.

Atakuwa nahodha wa timu inayowajumuisha watu nyota na wachezaji nyota wa sasa na waliostaafu katika mechi ya Soccer Aid kwa ajili ya kuchangisha pesa za kutumiwa na Unicef 10 Juni uwanjani Old Trafford, Uingereza. Kutakuwa na timu ya England na timu ya watu kutoka nje ya England (Dunia XI)

"Yeye ni mchezaji mzuri, vinginevyo hangekuwa akishiriki mazoezi nasi," mkurugenzi wa uchezaji wa Stromsgodset Jostein Flo alisema.

Flo amesema Bolt amepewa jezi nambari 9.58 - rekodi yake katika mbio za mita 100m.

Kuwasili kwake Stromsgodset kuliwashangaza wachezaji.

Wachezaji wa timu zitakazokabiliana mechi ya Soccer Aid

England

Robbie Williams, Olly Murs, Mo Farah, Paddy McGuinness, Michael Owen, Ben Shephard, Mark Wright, Wes Brown, Joe Wicks, David Seaman, Lee Mack, Phil Neville, Freddie Flintoff, Danny Murphy, Myles Stevenson, Jamie Redknapp na Robbie Fowler.

Wachezaji wa timu ya dunia (Dunia XI)

Usain Bolt, Clarence Seedorf, Robert Pires, Gordon Ramsey, Brendan Cole, Yaya Touré, Kevin Pietersen, Jaap Stam, Dan Carter, Patrick Kluivert, Edwin van der Sar, Eric Cantona na Ashley Fongho.

Flo, mchezaji wa zamani wa Sheffield United alisema: "Tuliwafahamisha kwamba kuna mchezaji ambaye angefika kufanya mazoezi na kwamba ana kasi ajabu - mlango ulifunguliwa, na Bolt akaingia. Wengi wao walipatwa na mshangao, hawakuamini."

STROMSGODSET

"Yeye ni mmoja wa wanariadha nyota zaidi katika historia, na bila shaka tunaweza kujifunza mengi sana kutoka kwake.

"Uwepo wake hapa bila shaka utawatia moyo wachezaji, wakufunzi na klabu yote."

Bolt alistaafu kutoka kwenye riadha Agosti mwaka 2017 baada ya mashindano ya ubingwa wa dunia jijini London.

Mwanariadha huyo ni shabiki sugu wa klabu ya Manchester United ya Uingereza na amekuwa akizungumzia hamu yake ya kutaka kucheza kandanda.

Bolt alitia saini mkataba na kampuni ya mavazi ya Ujerumani ya Puma ambao pia ni wadhamini wa Sundownd akiwa bado mdogo mwaka 2003.

Usain Bolt akifanya mazoezi na Mamelodi Sundowns

Amekuwa akiashiria hamu yake ya kuwa mwanakandanda baada yake kustaafu riadha, na anaamini kwamba anaweza kuwa sawa kiasi cha kuchezea timu ya taifa ya Jamaica.

Bolt alifanya mazoezi wiki moja na klabu ya Ujerumani ya Borussia Dortmund mwezi Machi mwaka huu.

Amekuwa akisema tangu akiwa mdogo alikuwa na ndoto ya kucheza kandanda.

Post a Comment

Kwa maoni na ushauri weka comment yako hapo chini:

Previous Post Next Post