Yanga Kuingia Kambini Leo Kwa Maandalizi ya Kuivaa Township Rollers



Baada ya Yanga kurejea jijini Dar es salaam jana jioni ikitokea mkoani Mtwara ilipocheza mchezo wa ligi kuu dhidi ya Ndanda FC, timu hiyo inatarajia kuingia kambini leo kuanza maandalizi ya kuivaa Township Rollers.

Yanga ambayo ilibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Ndanda kwa mara ya kwanza kwenye uwanja wa Nangwanda Sijaona, katikati ya wiki ijayo itakuwa na kibarua cha mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Township Rollers ya Botswana.

Taarifa ya klabu hiyo imebainisha kuwa wachezaji wake waliokuwa majeruhi wakiwemo viungo washambuliaji,  Juma Mahadhi na Mzimbabwe Thabani Kamusoko, mshambuliaji Mzambia Obrey Chirwa wote wamepona.     

''Tunaingia kambini leo na tutakuwa na siku nne za kujiandaa na mchezo wetu wa kimataifa dhidi ya Township Rollers utakaopigwa Machi 6 kwenye uwanja wa taifa jijini Dar es salaam'', imeeleza taarifa hiyo.

Benchi la ufundi la Yanga chini ya kocha George Lwandamina anayesaidiwa na Mzambia mwenzake Noel Mwandila pamoja na wazawa Nsajigwa Shadrack na Juma Pondamali ambaye ni kocha wa makipa limejipanga kuhakikisha wanapata ushindi mnono ili kujiweka sawa na mechi ya marudiano huko Gaborone.

Post a Comment

Kwa maoni na ushauri weka comment yako hapo chini:

Previous Post Next Post