Rostam Ataka Kuondoka Yanga Kocha Afunguka


Rostam Ataka Kuondoka Yanga Kocha Afunguka

KOCHA Mkuu wa Yanga, Mwinyi Zahera raia wa DR Congo, amefunguka kuwa alifanikiwa kuona kiwango cha Deus Kaseke kupitia mechi ya Simba, huku akisema Youthe Rostand ameomba kuondoka.



Hivi karibuni Yanga ilifanikiwa kumrejesha Kaseke kikosini kwao akitokea Singida ili kuongeza nguvu kwenye kikosi hicho ambacho kinasuasua.



Katika kudhihirisha kuwa hawakufanya makosa kumsajili mchezaji huyo, wikiendi iliyopita Kaseke aliifungia Yanga bao moja katika kipigo cha mabao 3-2 kutoka kwa Gor Mahia ya Kenya kwenye mchezo wa Kombe la Shirikisho Afrika uliopigwa katika Uwanja wa Taifa, Dar.



Akizungumza na Championi Jumatano, Zahera alisema kwa mara ya kwanza aliona uwezo wa Kaseke akiwa hotelini akiishuhudia mechi hiyo kwenye runinga na akaamua kufanya uamuzi wa kumsajili huku akiwa na matumaini ya kiungo huyo atakuwa msaada kikosini kwake.



“Kaseke kwa mara ya kwanza nilimuona kwenye mechi ya Simba na Singida, hapo nilikuwa hotelini naangalia mchezo huo kupitia ‘TV’ ndipo niliweza kumpigia simu kocha Mwandila (Noel) na kumuuliza yule mchezaji ni nani, akaniambia, nikasema namuhitaji kwenye kikosi changu, ndipo nikapata jibu kwamba aliwahi kucheza hapa.



“Lakini kwa kipindi hiki kifupi ambacho nimekaa naye, nimegundua ni mchezaji mzuri hasa kifiziki, akiendelea kupambana atafika mbali zaidi, kikubwa ni kuepuka yale makosa madogomadogo lakini atakuwa mchezaji tegemeo kwenye timu,” alisema Zahera.



Katika hatua nyingine, Zahera alisema jana Jumanne beki wake, Kelvin Yondani kwa mara ya kwanza alianza mazoezi na wenzake baada ya kukosekana kwa muda mrefu kutokana na mkataba wake kumalizika, huku akibainisha kwamba, kipa wa timu hiyo, Youthe Rostand hakutokea mazoezini huku taarifa zikidai alikutana na uongozi wa Yanga kuona uwezekano wa kuvunja mkataba wake ili aondoke kikosini hapo.

Post a Comment

Kwa maoni na ushauri weka comment yako hapo chini:

Previous Post Next Post